TANGAZA BIASHARA YAKO HAPA NA UONE FAIDA YAKE

Kwa Habari au Tangazo lolote la Biashara tuwasiliane kwa Simu 0713 - 581741 au 0755 - 863097.Email: robadio8@gmail.com

Tuesday, June 28, 2011

Mbunge ailipua Ikulu,

MBUNGE wa Chadema, Suzan Lyimo ameishangaa Serikali kwa kutenga mabilioni ya fedha kwa ajili ya ukarabati wa Ikulu ya Dar es Salaam kila mwaka, huku Serikali hiyo hiyo ikiendelea kusisitiza mikakati ya kuhamia Dodoma.

Akichangia mjadala wa bajeti kuhusu Makadirio ya Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu pamoja na ofisi zilizopo chini yake, kwa mwaka wa Fedha 2011/12 jana, Lyimo alisema haungi mkono hoja hiyo, mpaka apewe majibu ya kuridhisha ya sababu za Rais kushindwa kuhamia Dodoma na badala yake kuendelea kutenga kiasi kikubwa cha fedha kukarabati Ikulu ya Dar es Salaam.

Akitoa takwimu mbalimbali za bajeti ya Ikulu tangu mwaka 2001 hadi mwaka 2011, Lyimo alisema kwa kipindi hicho cha miaka kumi, Ikulu imekwishatengewa zaidi ya Sh50 bilioni, fedha ambayo kwa maoni yake, zinatumika vibaya.

"Siungi mkono hoja hii kwa sababu tatu; moja ni ukubwa wa Baraza la Mawaziri, mbili uonevu wanaofanyiwa wanafunzi wa elimu ya juu na tatu Serikali kutokuwa na mpango wa dhati wa kuhamia Dodoma," alisema Lyimo alipoanza kuchangia mjadala huo.

Kwa mujibu wa mbunge huyo wa Viti Maalumu, kitendo cha Serikali kuendelea kuliomba Bunge liidhinishe matumizi ya Sh10 bilioni kwa ajili ya ukarabati wa Ikulu ya Dar es Salaam katika kipindi cha mwaka 2011/2012, kinaonyesha kuwa haina nia ya dhati wala utashi wa kisiasa kutekeleza mpango wa kuhamia Dodoma.

"Tangu mwaka 2001 hadi 2011, Ikulu hiyo imetengewa Jumla ya Sh56 bilioni. Kila mwaka Serikali inaomba Sh2 bilioni, mwaka jana iliomba Sh7.2 bilioni na mwaka huu imeomba Sh10 bilioni," alilalamika Lyimo na kuendelea:

"Hivi ni kweli mabilioni hayo yanatengeneza Ikulu ya Rais tu pale Dar es Salaam? Na kama kweli ni Ikulu, kwa nini isitengenezwe Ikulu ya Chamwino ili Rais ahamie Dodoma?" alihoji

Lyimo alisema haoni mantiki kwa Rais kuendelea kuishi Dar es Salaam wakati mpango wa kuhamia Dodoma ulianza tangu mwaka 1976 na kila mara Serikali imekuwa ikiendelea kusisitiza mpango huo.

"Mheshimiwa mmoja hapa alipendekeza Spika ahamie Dodoma, mimi nasema sio Spika ni Rais ndiye anayepaswa kuja Dodoma. Na kama Rais anahamia Dodoma hakuna waziri atakayebaki Dar es Salaam. Tunamtaka pia Waziri Mkuu kuja Dodoma," alisema.

Baraza ni mzigo
Kuhusu Baraza la Mawaziri, Lyimo alisema ni kubwa kupita kiasi na kwamba Serikali inapaswa kulipunguza ili kupunguza matumizi yasiyokuwa ya lazima serikalini.

Alisema mawaziri 54 waliopo sasa, ni wengi mno na wanaiongezea mzigo wananchi ambao ndio wanaobeba jukumu la kuigharimia Serikali yao.

"Baraza la Mawaziri ni kubwa mno, wako 54 ukimjulisha na Rais, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu na Rais wa Zanzibar. Nchi tajiri kama Marekani ina mawaziri 15 tu, kwa nini Tanzania ambayo ni maskini iwe na mawaziri wote hao?" alihoji na kusisitiza, "tunaomba Serikali iliangalie upya baraza lake la mawaziri."

Katika hoja ya uonevu aliodai unafanywa na Serikali kwa wanafunzi wa Vyuo vya Elimu ya Juu, Lyimo alihoji sababu za wanafunzi kufukuzwa baada ya kufanya migomo na maandamano wakati kisheria, inaruhusiwa vyuoni.

Muungano watikisa
Katika hatua nyingine, hoja ya Muungano jana ilitawala mjadala huo unaoendelea bungeni baada ya wabunge kadhaa kutoka Zanzibar, kueleza kuwa bado una kero nyingi na hivyo kupendekeza uvunjwe.

Wakichangia mjadala huo kwa nyakati tofauti, wabunge hao walisema Muungano bado ni kero kwa Wazanzibari kwa kuwa kuna mambo mengi ya msingi ambayo yanatendeka bila kujali maslahi ya pande zote mbili.

Mbunge wa Mgogoni, Kombo Khamis Kombo alihoji namna haki inavyoweza kutendeka katika mazingira ya nchi hizi mbili kuungana kwenye wizara sita tu kati ya wizara 26 zinazounda Serikali ya Muungano.

"Seriklai hii ina wizara 26 na wizara za Muungano ni sita tu. Mambo yote yanayofanywa kwenye wizara ambazo sio za Muungano bajeti yake inapangwa na kutekelezwa na Serikali ya Muungano, sasa licha ya jambo hilo kuwa kikatiba, kutakuwa na usawa gani kati ya Zanzibar na Tanganyika?" alihoji.

Mbunge huyo alisema haamini kama Serikali ya Muungano ina nia ya dhati katika kutatua kero za muungano na kama ina nia ya kweli, iwajengee imani Wazanzibari kwa Waziri Mkuu kuzungumzia kero hizo wakati anajibu hoja za wabunge katika mjadala unaoendelea.

"Mheshimiwa Spika, katika mazingira haya, tunawahakikishia Wazanzibari kuamini kuwa Tanganyika (Tanzania Bara) inawadhalilisha. Zanzibar kuna mabalozi wanne tu tena wanapelekwa kwenye nchi za Kiarabu na sasa China amepaelekwa mheshimiwa Mapuri. Wazanzibari wana haki, uwezo na haki ya kupeleka wafanyakazi katika balozi,"alieleza.

Kombo alisema kitendo cha Serikali kupuuza mapendekezo ya kamati ya Nyalali, Shelukindo na Amina Salum Ally kuhusu kero za Muungano ni ishara tosha kwamba haina nia ya dhati kutatua kero hizo zinazolalamikiwa na Wazanzibari.

Maelezo hayo yaliungwa mkono na mbunge wa Micheweni (CUF), Haji Khamis Khai aliyeeleza kuwa Wazanzibari hawana imani na Muungano huo kwa kuwa wao ni maskini kuliko Tanzania Bara.

"Kama Zanzibari ni mzigo kwenu (Bara) tuvunje muungano huo, mtuache," alisema.

Alisema inaudhi Wazanzibari kuzungumzia kero za Muungao kila siku na Serikali ya Muungnao ikiendelea kuwa kimya bila kutoa kauli inayotekelezeka."Tunaomba Muungano uvunjwe na uundwe tena kama ni lazima," alisema.

Hii ni mara ya pili kwa wabunge kujadili hoja ya Muungano katika Mkutano huu wa nne unaondelea sasa. Mara ya kwanza hoja hiyo iliibuliwia na mbunge wa Chwaka (CCM), Yahya Kassim Issa ambaye aliliambia Bunge kwamba Muungano wa Tanzania Bara na Zanzibar, bado una sintofahamu nyingi.

Akichangia Hotuba ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda Kuhusu Mapitio na Mwelekeo wa Kazi za Serikali na Makadirio ya Matumizi ya Fedha ya Ofisi ya Waziri Mkuu na Bunge ya mwaka 2011/2012 jana, mbunge huyo alisema suala la Muungano bado lina utata unaopashwa kushughulikiwa haraka.

"Mheshimiwa Spika, Wakati Rais akitolea ufafanuzi suala hilo la Muungano alieleza kuwa Zanzibar ni nchi ndani ya nchi ya Tanzania lakini, Nje ya nchi, nchi ni Tanzania. Lakini mheshimiwa spika, mpaka leo vitabu hivi, bado vinaitambua Zanzibar kuwa ni mkoa kama ulivyo Kilimanjaro!"

"Mbona vitabu havitoki kubadilisha hilo ili Zanzibar isomeke kuwa ni nchi kama Rais alivyosema? Huu ni mzozo, Zanzibar kuonekana kama mkoa na sisi (Wazanzibari), hatutaki," alilalamika.

No comments: