TANGAZA BIASHARA YAKO HAPA NA UONE FAIDA YAKE

Kwa Habari au Tangazo lolote la Biashara tuwasiliane kwa Simu 0713 - 581741 au 0755 - 863097.Email: robadio8@gmail.com

Friday, July 8, 2011

Sitta nae Amtupia kombora Lowassa,ASEMA UAMUZI MGUMU HAUNA MAANA KAMA RUSHWA IMESHAMIRI NCHINI



KATIKA kile kinachoonekana kumjibu Waziri Mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa, Kaimu Waziri Mkuu, Samuel Sitta amesema, "Maamuzi magumu sawa, lakini hayana maana kwa nchi yoyote kama hakuna uadilifu.""Maamuzi magumu hayawezi kufanyika wakati rushwa ikiendelea kushamiri,"alisema Sitta ambaye pia ni Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki alipokuwa akijibu hoja za wabunge waliochangia hotuba ya makadirio ya ofisi ya Makamu wa Rais bungeni jana na kuongeza:

''Maamuzi magumu sawa, lakini hayana maana kwa nchi kama hakuna uadilifu..., suala hili sio ‘10 parecent’, hivi maamuzi magumu maana yake ni rushwa iendelee?’’ Kauli hiyo inaonekana kama ni kujibu hoja ya Lowassa ambaye alikuwa Waziri Mkuu wa kwanza katika utawala wa Awamu ya Nne wa Rais Jakaya Kikwete, ambaye alisema Serikali inasumbuliwa na ugonjwa wa woga katika kutoa uamuzi mgumu na matokeo yake mambo mengi hayaendi kama yalivyopangwa, hivyo kuitaka ibadilike.

Kwa mujibu wa Lowassa ni bora mtu ukalaumiwa kwa kufanya uamuzi mgumu kuliko kulaumiwa kwa kutofanya uamuzi na kwamba Serikali inapaswa kufanya uamuzi bila kujali matokeo yake huku akipendekeza kwa kuanzia, ikope kwa kutumia rasilimali za nchi na kuendeleza miradi mikubwa kama reli na bandari.

"Ni bora kulaumiwa kwa kufanya maamuzi kuliko kulaumiwa kwa kutofanya maamuzi kabisa,"alisema Lowassa na kuongeza:"Kuna ugonjwa wa kutokutoa maamuzi hapa na lazima tukubali kubadilike. Ni heri mtu ukosee kutoa maamuzi kuliko kukaa kimya kabisa, heri uhukumiwe kwa kutoa maamuzi kuliko ulaumiwe kwa kushindwa kutoa maamuzi,"alisema.

Ingawa kauli hiyo ya Lowassa ilishajibiwa na Waziri Mkuu Mizengo Pinda alipokuwa akihitimisha hotuba ya makadirio ya ofisi yake, jana Sitta, bila kumtaja Lowassa alisema, uamuzi mgumu hauwezi kufanyika wakati rushwa ikishamiri.

Sitta ambaye ni mbunge wa Urambo Mashariki alisema kuwa Mwalimu Julius Nyerere alisimamia suala la uadilifu ndio maana Tanzania ilitukuka.”Ulaji rushwa ndio unachelewesha maendeleo, Mwalimu alisimamia sana suala hili la uadilifu ambalo ndio linaloziharibu nchi za dunia ya tatu. Uadilifu ndio chanzo cha mikataba ya kitoto, maamuzi mabovu..., wanaomsema Mwalimu Nyerere na kumchukia wana lao jambo,’’ alisema Sitta.

Hoja ya Muungano
Awali wakati akijibu hoja mbalimbali, Sitta alisema nchi imekumbwa na giza na kwamba watu hawaelewi mambo mazuri yaliyomo katika Muungano.”Hatutoi taarifa vizuri kwa wananchi, tunatakiwa kueleza tulipotoka hali ilikuwaje, sasa basi nachukua nafasi hii kuyasema haya ambayo sio kama nayaamini mimi, ila mantiki yake ni ya wakati ule, sasa tunaweza kupima kama wakati huu yatafaa ama vipi,’’ alisema Sitta.

Sitta ambaye pia amewahi kuwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alianza kufafanua suala la muungano linaloihusu wizara yake katika mchakato wa kuunganisha Afrika Mashariki.”Masuala ya Afrika Mashariki huwa tunajadili pamoja na Zanzibar, hakuna jambo tunalokwenda kujadiliana bila uwepo wa ushiriki wa Zanzibar.
Tunafanya mikutano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Muungano,’’ alisema Sitta.Alifafanua kwamba Serikali hizo mbili hukaa pamoja na kuweka misimamo yao kuanzia ngazi ya mawaziri mpaka wataalam wa sekta mbalimbali sambamba na Serikali ya umoja wa kitaifa.

Alisema kutokana na ushiriki huo imeibuka miradi mbalimbali ambayo imeanza kutekelezwa kwa kuombewa fedha katika benki ya maendeleo ya Afrika na kwamba fedha hizo sio kama zinaombwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pekee bali na sekretarieti ya Afrika Mashariki.”Kuna mradi wa ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Karume ambapo fedha za ujenzi huo wa uwanja wa kimataifa zinatafutwa pamoja na ujenzi wa Bandari ya Mavubi na ujenzi wa chelezo katika bandari ya Dar na Zanzibar.

Tunatarajia mwaka huu wa fedha, Benki ya Afrika itakuwa imeshatujibu,’’ alisema Sitta.Alisema kuwa hata katika ofisi yake kuna wafanyakazi kutoka visiwani Zanzibar akiwamo Naibu Waziri wake, na watumishi waandamizi wanne.

Kuchanganya mchanga
Akizungumzia tukio la kuchanganywa kwa mchanga wa Tanganyika na Zanzibar lililomaanisha muungano uliozaa Tanzania, ambalo baadhi ya wabunge wamelilalamikia kutokana na kuwa katika uchanganyaji huo aliyeonekana ni rais wa Tanganyika (Nyerere), Sitta alisema hali hiyo ilitokana na makubaliano baina ya Nyerere na Karume.
Alisema baada ya makubaliano katika Bunge lililokuwa na wawakilishi wa Zanzibar pamoja na Baraza la Mapinduzi la wakati huo, rais wa Zanzibar wakati huo, Abeid Aman Karume alimpa heshima rais wa Tanganyika, Julius Nyerere kuchanganya mchanga huo.

Alisema pia walikubaliana kwamba Rais wa kwanza wa Muungano awe Nyerere na kwamba ndio atakayechanganya mchanga huo.”Kuna vijana wawili walitokea Zanzibar na wengine wawili walitokea Bara kwa ajili ya tukio lile na katika kuchanganya mchanga alipewa heshima Nyerere, uamuzi huo unaweza kuukosoa, lakini mantiki yake ndio hiyo.

Kulikuwa hakuna ulazima wa kumtoa Karume Zanzibar aje kuchanganya mchanga,’’ alisema Sitta.Akizungumsia suala la Rais wa Zanzibar kutokuwa Makamu wa Rais wa Muungano, Sitta alisema suala hilo lilifanyika ili kuepuka Zanzibar kutoa makamu tu.”Kama ikiwekwa katika katiba makamu atokee Zanzibar basi ingetokea rais na makamu wote wangetokea Zanzibar, suala hili ndio lilitazamwa kwa mtindo huo,’’ alisema Sitta.Aliongeza, “Ndio maana Mzee Mwinyi alikuwa rais na alitokea Zanzibar’’.

Hoja ya MafutaSitta alisema mpaka wa Tanzania na Zanzibar ni kilomita 240 mashariki mwa visiwa hivyo na kwamba katikati ya mpaka huo, kuna mkondo (Zanzibar channel), hivyo kuna uwezekano mkubwa mafuta yakapatikana ndani ya mpaka huo.”Suala la uchumi sio la Muungano..., lengo si kuziweka rasilimali chini ya muungano bali ni kuangalia uwezekano wa kupatikana mafuta ndani ya eneo la ndani ya Jamhuri ya Muungano,’’ alisema Sitta.

Aliongeza kuwa; “Miamba haina mipaka, inawezekana chini ya bahari kati ya Tanga na Zanzibar kukawa na mafuta sasa ya nani?’’ alihoji."Ndio maana ikasemwa suala hilo liwe la muungano ikiwa ni pamoja na kugawana kistaarabu kuepusha ugomvi, hata kama tukitengana leo lazima tuelezane ili tusigombane,’’.

Mikataba ya kimataifa
Kuhusu mikataba ya kimataifa, Sitta alisema sio kweli kwamba serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inaiminya Zanzibar na kuonya kuwa tafsiri hiyo haifai."Sheria za kimataifa inailazimisha Zanzibar ipitie katika muungano. Tulijaribu kuiombea Zanzibar iingine katika Jumuiya ya Nchi za Kiislam (OIC), lakini walitujibu kuwa suala hilo haliwezekani kwa kuwa Zanzibar sio nchi,’’ alisema Sitta.

Alisema kuwa katika Umoja wa Mataifa kinachotambulika ni kitu kimoja ambacho ni Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kwamba suala hilo linashindikana kwa sababu ya sheria za kimataifa na si Serikali ya Muungano. Serikali tatuSitta alisema kwa akili ya kawaida tu suala la kuwepo kwa Serikali tatu ni njia nyepesi ya kuua Muungano.

Alisema kwa sasa upande wa pili wa muungano haugharamii nishati ya umeme, hivyo kitendo cha kuwa na Serikali ya Tanganyika kutaibua mvutano kwa kuwa nao hawatakubali kuona hali hiyo.”Upande wa pili hawagharamii umeme kwa kiwango kinachotozwa Bara, kungekuwa na Serikali ya Tanganyika ingelipiza kisasi. Zanzibar hawalipii umeme na wanadaiwa bilioni 50, wana gharama nafuu tena kwa sababu ya S mbili, ingekuwa Serikali tatu hali ingekuwa tofauti,’’ alisema Sitta.

No comments: