TANGAZA BIASHARA YAKO HAPA NA UONE FAIDA YAKE

Kwa Habari au Tangazo lolote la Biashara tuwasiliane kwa Simu 0713 - 581741 au 0755 - 863097.Email: robadio8@gmail.com

Thursday, July 7, 2011

MWANZA NA DAR HAKUKALIKI.MABOM MABOM MABOM, RISASI RISASI MTINDO MMOJA


Gari likiwa limechomwa moto katika mkoa wa Mwanza kufuatia vurugu zilizotokea kati ya jeshi la polisi na wafanya biashara wadogo(wamachinga)


RISASI za moto, mawe na mabomu ya machozi jana viliyateka majiji ya Mwanza na Dar es Salaa, kufuatia kuibuka kwa vurugu zilizowalazimisha polisi kutumia silaha za moto katika miji hiyo.

Jijini Mwanza mapambano yalikuwa ni baina ya wafanyabiashara wadogo maarufu kama wamachinga, ambao waliingia vitani na askari polisi hali iliyosababisha maduka, ofisi na huduma mbalimbali kusimama kwa muda wa saa saba.

Katika vurugu hizo askari Polisi walikuwa wakihaha kila kona ya mji kuzuia uharibifu wa mali kutokana na watu wanaodaiwa kuwa wafanyabiashara ndogondogo (machinga) kuchoma magari moto, kuvunja magari vioo na maduka huku wengine wakipora mali madukani na hotelini.

Vurugu hizo zilianza majira ya saa 3:45 asubuhi baada ya wamachinga kumiminika katika mitaa ya Makoroboi, Rwagasore na Lumumba na kukuta polisi na mgambo wa jiji wametanda kuzuia wasifanye biashara. Askari hao walifika katika mitaa hiyo kuanzia majira ya saa 12: 00 asubuhi.

“Polisi waliowahi asubuhi walikuwa wachache, na kutokana na machinga kuwa wachache muda huo walifanikiwa kuwazuia, lakini kumbe machinga walikuwa wakikusanyika, kadri muda ulivyokuwa ukisonga,”alisema mmoja wa wafanyabiashara na kuongeza:

“Baadaye walifika machinga wengi, na ndipo walipoanza kuzomeana na polisi na kisha kuwarushia mawe polisi kiasi cha kuzidiwa nguvu”.

Kutokana uchache wao, polisi walizidiwa nguvu na wamachinga waliokuwa wakiwashambulia kwa mawe, hivyo polisi hao kuanza kutimua mbio huku wakitumia radio za mawasiliano kuomba msaada kwa wenzao.

Kati ya askari hao, ni wawili tu waliokuwa na silaha za moto na wengine walikuwa na virungu, hivyo ikawa rahisi kwa wamachinga kuwazidi nguvu kwa kutumia mawe.

Kauli ya polisi
Taarifa ya kuzidiwa kwa askari hao zilimfanya kamanda wa polisi mkoa wa Mwanza, Simon Sirro kutembelea eneo la tukio na kuzungumza na machinga na kuagiza askari wake kuondoka eneo hilo la Makoroboi, kauli iliyoshangiliwa na wamachinga.

Baadaye Sirro aliwaambia waandishi wa habari kuwa jeshi lake liliombwa kusaidia mgambo wa jiji kuzuia wamachinga kufanya biashara katika baadhi ya maeneo wasiyoruhusiwa na walifanya hivyo, lakini ghafla hali ilibadilika na kutolewa taarifa kwamba waruhusiwe.

“Hatuwezi kufanya kazi katika migongano, sisi tumekwenda kuzuia wamachinga huku nyuma tena ikatoka kauli kuwa hilo eneo waendelee tusiwazuie, sasa nilichoamua ni kuwaondoa askari wangu, wakishakubaliana wao watatuambia la kufanya,” alieleza kamanda Sirro.

Maduka yaporwa
Baada ya Sirro kuondoka, wamachinga walizusha upya vurugu ambapo safari hii kundi moja likiwa linamsindikiza kamanda na kumuimbia ‘Sirro..Siroo..’ kundi lingine lilianza kuvamia maduka na kupora mali za watu.

Miongoni mwa maduka yaliyopowa ni Zara Solar Ltd mali ya Mohamed Papia, ambako wavamizi wapatao 50 waliingia dukani humo na kupora fedha na vifaa mbalimbali vya umeme baada ya kuvunja vioo vya duka hilo pamoja na mlango.

“Wameingia kundi, wamefanya wanavyotaka, kila aliyeingia amebeba alichoweza… wamebeba mpaka hela,” alieleza Papia.

Wakati polisi wakutuliza ghasia katika duka la Zara, kundi lingine la wamachinga lilivamia Mwanza Hosipitali iliyopo mtaa wa Rufiji ambako walivunja vioo vya jingo hilo na kuharibu jenereta.

Kundi jingine lilivamia Hotel za Florida ambako watu hao walipora viti, meza na vinywaji, huku hoteli ya Kembice iliyopo katika mtaa huo ikipondwa kwa mawe na vioo vyake kuvunjwa.Katika vurugu hizo mgari kadhaa pia yaliharibiwa vibaya.

Habari zilizopatikana jijini Mwanza zilisema wavamizi hao walisikika wakisema watakuwa wakipambana na wafanyabiashara wenye asili ya kiasia kutokana na kuamini kuwa wao ndiyo wamekuwa wakifaidi kwa kufanya biashara salama wakati wao wakipigwa na kuporwa vitu vyao.

“Leo wameingia kwangu kupora wakisema tunarudisha mtaji wetu ambao tumekuwa tukiporwa na jiji, hii ni hatari sana,” alieleza mmoja wa wafanyabiashara hao.

Majeruhi wa Risasi
Habari kutoka Hospitali ya mkoa wa Mwanza, Sekou Toure zimeeleza kuwa walipokea majeruhi wanne ambapo wawili hali zao zilikuwa mbaya hivyo kuhamishiwa hospitali ya rufaa ya Bugando kwa matibabu zaidi.

Mmoja wa wauguzi wa hospitali hiyo ambaye hakutaka kutajwa jina lake, aliwataja majeruhi hao kuwa Omari Abdalah (25) mkazi wa Nyashana ambaye ni fundi wa Koroboi, Kelvin Jeremia (16) ambaye amejeruhiwa kwa risasi mgongoni, Pastory Brison (25) ambaye alijeruhiwa kwa risasi kiunoni na mwingine aliyefahamika kwa jina la Juma ambaye alifikishwa akiwa hajitambui.

Muuguzi huyo alisema Juma na Pastory walihamishiwa hospitali ya rufaa ya Bugando kutokana na majeraha yao kuwa makubwa, hivyo kuhitaji matibabu zaidi.

Kauli ya Jiji
Kaimu Mkurugenzi wa Jiji la Mwanza, Frances Mkabenga alisema mpango wao ulikuwa ni kuwahamisha wamachinga hao kutoka eneo la Makoroboi kwenda katika eneo lililotengwa kwa ajili ya shughuli hizo.

“Tulikuwa na kazi mbili leo (jana) ya kwanza ni kuhamisha machinga na kituo cha daladala, askari waliwahi asubuhi na mapema sana na tulifanikiwa, lakini ghafla saa nne walitueleza kuwa kuna vurugu zimezuka na sasa hali ndiyo hii, hatujui nini kilifanya vurugu kuzuka pengine labda kuna mtu kawashawishi, hatujui,” alieleza kaimu mkurugeni huyo.

Vurugu Manzese
Naye Hussein Issa anaripoti kutoka Dar es Salaam kuwa, risasi za za moto, mabomu ya machozi na kuvunjwa kwa kituo cha polisi, ni matukio yaliyotokea jana baada ya wananchi kukataa kuzikwa kwa mwili wa marehemu kwa madai kwamba amechukuliwa kwa imani za ushirikina (msukule) .

Tukio hilo lilitokea majira ya saa tisa alasiri nyumbani kwa marehemu, Bakari Machemba (22) ambaye alifariki baada ya kuanguka akiwa kwenye mazoezi ya mpira wa miguu.

Milio ya risasi ilisikika na mabomu ya machozi kupigwa, hivyo kusababisha wakazi wa eneo la Manzese Mpakani kukimbia ovyo.

Katika tukio hilo kituo cha polisi cha Mpakani kikuvunjwa milango na askari kukimbia baada ya kundi la vijana kuvamia na kuwatoa watuhumiwa wote. Pia kundi hilo lilichoma pikipiki ya polisi ambayo iliteketea.

Baba wa marehemu aliyejitambulisha kwa jina la Kazumari Machemba alisema, mtoto wake alianguka akiwa mpirani na kwamba alipoteza maisha walipokuwa wakimpeleka hosipitalini kwa matibabu.

Alisema kabla ya kwenda hosipitali marehemu Bakari alifikishwa nyumbani akiwa ana anaweweseka.

"Alikuwa anaweweseka kama kuku kwa kweli roho iliniuma sana ila sasa niliogopa kumpakiza kwenye gari kwasababu alikuwa anarusha miguu,"alisema.

Aliongeza kwamba mara baada ya kufariki walipeleka mwili katika hospitali ya Mwananyamala ambako ilithibitishwa kitabibu kuwa kafariki dunia na wao kuanza shughuli za mazishi.

Mazishi
Alisema waliamua kuzika jana, hivyo kuamua kumswalia marehemu katika msikiti wa Kione na kwamba
walipokuwa wakipakiza mwili wa marehemu kwenda makaburini, ghafla kundi la watu likavamia na kudai kwamba marehemu hakufariki, hivyo kutaka mazishi yasifanyike hadi uchunguzi ufanywe.

Kwa mujibu wa baba huyo wa marehemu, kauli hiyo ilimfanya aombe msaada polisi ndipo wakafika na kumpakia kuelekea Mwananyamala kumuhifadhi tena.

"Hali haikuwa nzuri kwa kweli na mpaka sasa nashindwa hata kuelewa kwanza huyu ni mwanangu mwenyewe wa kumzaa sina mwingine wale waliokuwa wanauzuia huu mwili ni wahuni tu,"alisema.

Alisema hajui lini atamzika mwanaye huyo kutokana na hali iliyojitokeza kwenye mazishi hayo.

HABARI NA PICHA KWA HISANI YA GAZETI LA MWANANCHI

No comments: