TANGAZA BIASHARA YAKO HAPA NA UONE FAIDA YAKE

Kwa Habari au Tangazo lolote la Biashara tuwasiliane kwa Simu 0713 - 581741 au 0755 - 863097.Email: robadio8@gmail.com

Wednesday, June 22, 2011

Mhindi aliyeua Mtanzania kunyongwa

MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imemhukumu kunyongwa kwa kamba hadi kufa raia wa India Vinoth Praveen kwa kosa la kumchoma visu hadi kufa Mtanzania, Abdul Basit.

Hukumu hiyo ilitolewa jana na Jaji Dk. Fauz Twaibu aliyesema kwamba mahakama imeridhishwa na ushahidi uliotolewa na upande wa Jamhuri.

Katika kesi hiyo ya jinai namba 83/2009 upande wa Jamhuri uliwakilishwa na Wakili wa Serikali Shadrack Kimaro, wakati upande wa utetezi uliwakilishwa na Wakili wa kujitegemea Majura Magafu.

Jaji Dk.Twaibu alisema kwa mujibu wa shahidi wa upande wa Jamhuri Inspekta Mapunda, aliyeieleza mahakama hiyo kwamba aliandaa maelezo ya onyo yaliyotolewa na mshtakiwa ambaye alikiri kufanya mauaji hayo.

Aidha, mshtakiwa alimueleza shahidi huyo kwamba hawezi kumruhusu mtu wake wa karibu kusikiliza anachomueleza shahidi huyo kwa sababu wakati anafanya mauaji hayo alikuwa peke yake na kwamba alifanya hivyo kwa kuwa shahidi huyo alionyesha kumjali.

“Pia kwa mujibu wa ungamo la mshtakiwa alilotoa mbele ya mlinzi wa amani (hakimu) alikiri kutenda kosa hilo kwa sababu mshtakiwa huyo alikuwa akimdai marehemu dola 20,000 za Marekani ambazo walikubaliana zirejeshwe kwa mshtakiwa katika kipindi kisichozidi mwaka mmoja lakini marehemu alishindwa kumfanya hivyo ndipo mshtakiwa akaamua kumuua.

“…Kwa ungamo hilo la mshtakiwa mbele ya mlinzi wa amani, maelezo ya onyo aliyochukuliwa na polisi ambayo amekiri kutenda kosa hilo na yalipokelewa na mahakama hii kama vielelezo na ushahidi wa mazingira wa kesi hii umethibitisha mshtakiwa alikuwa na dhamira ya kutenda kosa hilo.

“Mahakama hii inatamka wazi kuwa inakubaliana na vilelezo hivyo kuwa ni kweli mshtakiwa huyo alimuua kwa kukusudia mshtakiwa huyo na kwamba adhabu ya mtu anayepatikana na kosa la mauaji hapa nchini ni moja tu, kunyongwa kwa kamba hadi kufa… hivyo mahakama hii inakuhukumu wewe Plaveen adhabu ya kunyongwa hadi kufa,” alisema Jaji Dk.Twaibu.

Ilidaiwa mahakamani hapo kuwa Februali 6 mwaka 2009 eneo la Kipata Kata ya Kariakoo jijini Dar es Salaam, mshtakiwa alimuua marehemu kwa kumchoma visu na mshale mgongoni, tumboni, shingoni na mdomoni kisha kuuweka mwili wake kwenye begi na kuutelekeza kwenye jengo la Harbours View ambayo awali liliitwa JM ALL jijini Dar es Salaam.

No comments: