TANGAZA BIASHARA YAKO HAPA NA UONE FAIDA YAKE

Kwa Habari au Tangazo lolote la Biashara tuwasiliane kwa Simu 0713 - 581741 au 0755 - 863097.Email: robadio8@gmail.com

Friday, June 17, 2011

MBOWE KUVUNJA BARAZA LA MAWAZILI KIVULI

BARAZA la mawaziri kivuli lililo na wabunge kutoka Chadema pekee, huenda likavunjwa na kuundwa jipya litakalojumuisha wabunge wa vyama vingine vya upinzani.

Kambi ya Upinzani bungeni inaongozwa na Freeman Mbowe na Naibu wake, Zitto Kabwe sasa inafanya mazungumzo na wabunge wa vyama vingine vya upinzani ikiwa ni hatua ya kutaka kushirikiana.

Ikiwa viongozi hao watafikia mwafaka, Mbowe atalazimika kufumua upya baraza lake la mawaziri ili kuwajumuisha wabunge wa vyama vingine vya upinzani.

Mchakato wa kuwashirikisha wabunge hao ulianza kwa Mbowe pamoja na Zitto kukutana na wabunge wa vyama vya NCCR Mageuzi, David Kafulila na TLP, Augustine Mrema mwishoni mwa wiki iliyopita katika Ofisi za Kambi ya Upinzani, bungeni, Dodoma.

Katika kikao hicho, pia walialikwa Wabunge wengine wa upinzani, Mohamed Habib Mnyaa (Mkanyageni-CUF) na John Cheyo (Bariadi Mashariki -UDP), lakini hawakuhudhuria kutokana na kuwa nje ya Mkoa wa Dodoma kikazi.

Mnyaa alikuwa na safari ya kibunge nchini Angola na Cheyo alikuwa mkoani Shinyanga ambako alikuwa na katika shughuli zinazohusiana na masuala ya kilimo cha pamba na uuzaji wa zao hilo.

Mwishoni mwa wiki hii Mbowe alikaririwa akisema kuwa mazungumzo hayo yameanza na kwamba wazo ni kuunganisha nguvu za wapinzani na kuwa na mtazamo mmoja wa masuala ya kitaifa kama vile bajeti ya nchi na mengine.

"Niseme tu kwamba kweli tuliwaomba wenzetu kukutana nao. Kama nilivyoahidi wakati nilipotangaza baraza langu la mawaziri kivuli kwamba suala la ushirikiano na wapinzani wegine ni la muda, hivyo tumeona ni vizuri kuanza sasa," alisema Mbowe.

"Mrema na Kafulila tulizungumza nao na tuliwaeleza nia yetu hiyo, sasa tunachosubiri ni mawazo kutoka kwao kwani sisi tayari tulishaweka hoja mezani, naweza kusema kwamba hapo ndipo tulipofikia hadi sasa," alisema Mbowe.

Mbowe ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chadema alisema wanatafuta fursa nyingine ya kukutana na wenzao hao ili kuendeleza mazungumzo, ikiwa ni pamoja na wale wa UDP na CUF ambao hawakuweza kushiriki katika kikao cha kwanza.

Jitihada za kuwaunganisha wapinzani wote bungeni, zimekuja wakati kambi hiyo ikitakiwa kutekeleza jukumu la kutunga kanuni za kuiongoza, suala ambalo Mbowe alisema linapewa nafasi ya kwanza hivi sasa ili kuweka utaratibu wa uendeshaji.

Kanuni za kambi rasmi ya upinzani bungeni lazima ziwatambue wabunge wote wa upinzani ikiwa ni pamoja na Kamati tatu za Hesabu za Serikali zinazoongozwa na wabunge wa kutoka upinzani.

Kamati hizo ni ile ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC), ambayo hivi sasa inaongozwa na Mrema, Hesabu za Serikali Kuu (PAC), ambayo inaongozwa na Cheyo na ile ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC), inayoongozwa na Zitto.

Kwa maana hiyo, taarifa zozote za kamati hizo lazima zifike kwa kiongozi rasmi wa kambi ya upinzani bungeni kabla ya kuwasilishwa katika vikao vya Bunge na hilo ni miongoni mwa mambo ambayo mchakato wa sasa wa kuwaweka pamoja wabunge wa upinzani unalenga kulitekeleza kwa ufanisi.

Mbowe alipotangaza orodha ya mawaziri kivuli, Februari, 13 mwaka huu alisema mawaziri hao 29 wanatoka Chadema tu kwa kuwa mawasiliano na vyama vingine yalikuwa bado hayajakamilika.

Chadema ni chama cha upinzani pekee kilichotimiza masharti yatokanayo na kanuni ya 14 fasili ya (4) ya kuchagua kiongozi wa kambi ya upinzani bungeni, hivyo kumpa Mbowe nafasi ya kuunda Baraza la Mawaziri Kivuli kutoka Chadema peke yake.

“Ni matumaini yangu kuwa hapo siku za usoni na baada ya kuelewana na kuridhiana na wenzetu, nitaweza kuunda baraza litakaloweza kushirikisha vyama vingine kutoka kambi rasmi ya upinzani bungeni,” alisema siku alipotangaza baraza hilo.

Hata hivyo, mmoja wa mawaziri hao, Leticia Nyerere aliyekuwa akiongoza Wizara Kivuli ya Mazingira alijiuzulu wiki iliyopita, akisema kuwa anawaachia wengine fursa ya kuongoza badala ya kung'ang'ania madaraka peke yake.

Kafulila na Mrema

Akizungumzia suala hilo, Kafulila ambaye ni Mbunge wa Kigoma Kusini alisema:
"Naona ni wazo zuri wala hakuna shida, kweli tumeshiriki katika kikao hicho, lakini nadhani bado ni mapema mno kusema ni nini kitakachotokea,"alisema Kafulila ambaye kabla ya kuhamia NCCR Mageuzi alikuwa mwanachama wa Chadema.

Alisema binafsi haoni ubaya wa kushirikiana na Chadema ikiwa wapinzani wana malengo yanayofanana ya kuwawakilisha wananchi, lakini pia kuibana Serikali itekeleze wajibu wake kwa umma.

Hata hivyo, alisema ushirikiano huo utawezekana ikiwa kutakuwa na maridhiano ya pamoja ya jinsi ya kuendesha kambi hiyo ili kulinda demokrasia na kuheshimu maoni ya pande zote hata pale kunapokuwa na mitazamo tofauti miongoni mwao.

Kwa upande wake, Mrema alisena: "Siyo jambo baya, ni zuri tu kwani kushirikiana na Chadema hatujaanzia hapa (bungeni), tumeanzia kule katika Halmashauri ya Moshi, ile Halmashauri inaogozwa na Chadema kwa kushirikiana na TLP."

Hata hivyo, alisema Chadema wamechelewa sana kutoa wazo hilo kwani fursa ilikuwapo tangu mwanzo na wakashindwa kuitumia kwa maelezo kwamba yeye (Mrema) ni kibaraka wa CCM.

"Jamani hata kama wanaamini kwamba mimi ni kibaraka wa CCM basi wangewaheshimu wananchi wa Vunjo ambao walinipigia mimi kura na kunichagua kuwa mbunge, kule Moshi Vijijini mbona tuna ndoa na mambo yanakwenda vizuri?” Alihoji Mrema na kuongeza:

"Kimsingi mimi sina matatizo, maana ushirikiano ni kitu kizuri sana hasa kwa maendeleo ya wananchi, sisi sote ni wapinzani kwa hiyo nadhani hakuna tatizo tukishirikiana na kuheshimiana."

Alisema anasubiri vikao vinavyofuata ili kuona hitimisho la majadiliano yanayoendelea miongoni mwao.

Kambi ya pamoja

Wakati Chadema kikianza mchakato wa kuwashirikisha wabunge wengine wa upinzani katika kuongoza kambi hiyo, kumekuwa na tofauti za kimtizamo kuhusu masuala mbalimbali yanayojitokeza ndani ya Bunge.

Miongoni mwa masuala hayo ni hoja inayotaka kufutwa kwa posho za vikao kwa wabunge na watumishi wengine wa umma. Chadema na NCCR-Mageuzi wanaonekana kuunga mkono suala hilo, hali CUF wakionyesha kuwa tofauti na msimamo huo.

Tofauti hiyo ilijitokeza juzi wakati Mnyaa alipouliza swali kwa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda akihoji iwapo Serikali haioni umuhimu wa kuwachukulia hatua za kisheria watu wanaovunja Katiba kwa kutaka kufutwa kwa posho ambazo kimsingi zipo kwa mujibu wa Katiba na sheria za nchi.

No comments: