TANGAZA BIASHARA YAKO HAPA NA UONE FAIDA YAKE

Kwa Habari au Tangazo lolote la Biashara tuwasiliane kwa Simu 0713 - 581741 au 0755 - 863097.Email: robadio8@gmail.com

Saturday, June 25, 2011

Dk Slaa amponda Lowassa ,ASEMA anawakejili Watanzania, ni sehemu ya matatizo



KATIBU Mkuu wa Chedema Dk Wlibroad Slaa ameunga mkono kauli ya Mbunge wa Monduli,Edward Lowassa na kumponda kuwa mbunge huyo ni sehemu ya matatizo yanayoikabili Tanzania hivi sasa.

Dk Slaa alisema kuwa Lowassa hakupaswa kutoa kauli hiyo kwa kuwa naye ni mmoja wa viongozi waliokuwa madarakani katika Serikali ya awamu ya nne, ambao hawakufanya vizuri hadi alipoamua kuachia madaraka kwa kujiuzulu.


Dk Slaa alitoa kauli hiyo jana alipokuwa akizungumza na wanafunzi wa Chuo kikuu cha Ualimu Dar es Salaam (DUCE), katika ukumbi wa TCC Changómbe Dar es Salaam. "Naiunga mkono kauli yake, lakini sio yeye, kwa sababu yeye mwenyewe ni miongoni mwa viongozi waliokuwa madarakani kipindi kile."

Alisema kimsingi ni kweli kuna matatizo ya usafiri wa reli, msongamano na makontena bandarini na ujenzi wa bandari na taifa kukabiliwa na mgawo wa mara kwa mara wa umeme uliodumu tangu mwaka 2006, lakini akasema kuna watu waliotakiwa kuyazungumza siyo Lowassa. Akizungumza katika mahojiano na Mwananchi Jumapili baada ya mkutano huo, Dk Slaa alisema kauli ya Lowassa ni kama kejeli kwa Watanzania na kwa viongozi walioko madarakani kwa sababu na yeye ni miongoni mwa waliokuwa madarakani

Aliongeza kwamba, kauli ya Lowassa ambaye pia ni Mbunge wa Monduli kusema Serikali inasumbuliwa na ugonjwa wa woga katika kutoa uamuzi mgumu ni ya kejeli kwa kuwa hata yeye alikuwa mtendaji mkuu wa serikali. Lowassa, ambaye alikuwa Waziri Mkuu wa kwanza katika utawala wa awamu ya nne, aliitaka Serikali hiyo kubadilika na kuwa na maamuzi magumu alitoa kauli hiyo bungeni wakati akichangia hotuba ya mapato na matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu ya mwaka 2011/2012.

Alisema kuwa ni bora kulaumiwa kwa kufanya uamuzi mgumu kuliko kulaumiwa kwa kutofanya uamuzi na kwamba, Serikali inapaswa kufanya uamuzi bila kujali matokeo yake. "Ni bora kulaumiwa kwa kufanya maamuzi kuliko kulaumiwa kwa kutofanya maamuzi kabisa," alisema Lowassa.

Aliongeza, "Kuna ugonjwa wa kutokutoa maamuzi hapa na lazima tukubali kubadilike. Ni heri mtu ukosee kutoa maamuzi kuliko kukaa kimya kabisa, heri uhukumiwe kwa kutoa maamuzi mabya kuliko ulaumiwe kwa kushindwa kutoa maamuzi." Naye Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk Azaveri Rwaitama alisema kwamba kauli ya Lowassa ni sawa na kiini macho kwa sababu yeye mwenyewe ni wa upande huo wa Serikali. Alisema wakati wa kipindi chake uwaziri mkuu, Lowassa aliyaona matatizo yote ya nchi, lakini alishindwa kuyakabili.

Rwaitama alisisitiza: Anachokisema Lowassa ni kiini macho.” Alisema Watanzania hawataki kuongozwa na watu wanaotaka umaarufu bali wanataka kuongozwa na wachapa kazi na siyo vinginevyo. Alisema kauli ya Lowassa inaonyesha wazi kuwa kuna ushindani unaendelea ndani ya serikali hali aliyodai inaweza kuleta mtafaruku mkubwa baadaye. "Mimi sina chama, awali nilikuwa TANU, lakini niliirudisha kadi baada ya kuona hakuna maelewano mazuri ndani ya chama, hivyo kwa sasa nipo tu bila ya chama'' alifahamisha Aliongeza kwamba haitakiwi kuruhusu vikundi ndani ya tabaka tawala kwani linaweza kuharibu nchi kabisa. Alisema huu sio muda wa kuongozwa na viongozi wanaotaka kuchukua nchi kiujanjaujanja kwani matokeo yake yatakuwa sio mazuri hapo baadae.

Maandamamo
Katika hatua nyingine, Dk Slaa amewaambia wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Ualimu Chang'ombe (DUCE) kuwa kuandamana ni haki yao na ya kila raia wa Tanzania. Dk Slaa ametoa kauli hiyo huku taifa likiendelea kukabiliwa na migomo na maandamano maeneo mbalimbali. Hata hivyo alisema kwamba ingawa yeye hawezi kuchochea vurugu, lakini wananchi kufanya maandamano si jambo la ajabu, pale wanapoona kuwa haki na amani havifuatwi katika nchi yao. Alisisitiza kwamba kila mtanzania ana haki ya kuishi, kuheshimika, kusema na kushiriki katika maamuzi. “Tatizo sisi tukisema ukweli tunaambiwa tunachochea wanafunzi na wananchi kuandamana…., sasa tusiposema ukweli huu tutausemea wapi; hiyo ndio kazi ya siasa, Serikali na Jeshi la Polisi wanatakiwa kulijua hili.

Hata hivyo aliwaonaya wanafunzi hao akisema: Ukiandamana kwa ushabiki wangu wewe hufai kuitwa mwanachuo.”
Dk Slaa ambaye alikuwa akitoa mifano mbalimbali inayoweza kumsukuma mtu kuandamana alisema kuna upotoshaji mkubwa katika upimaji wa maendeleo ya nchi. Alisema siku zote anayeambiwa ukweli huumia huku akilishukia Jeshi la Polisi nchini kuwa kupiga marufuku maandamano ni upuuzi kwa kuwa kupitia maandamano baadhi ya mambo yamewekwa sawa ikiwa ni pamoja na bei za bidhaa mbalimbali. Huku akitoa mfano wa baadhi ya vitabu vilivyoandikwa na Mwalimu Julius Nyerere mwaka 1968 vilivyogusia haki, amani na usawa, alisema amani sio ukosefu wa nchi kuwa na mapigano bali ni Watanzania kujitawala wenyewe kuwa na uhuru wa kufanya mambo yao bila kuingiliwa na mtu. Alisema: “Kujenga barabara, nyumba za kifahari na shule sio maendeleo bali hivyo ni vyombo vya kuleta maendeleo tena kama vyombo hivyo vitatumika kweli kuleta maendeleo.”

No comments: